UNHCR YASEMA TANZANIA HAIKUWAFUKUZA WAKIMBIZI- Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR, ofisi ya Tanzania limekanusha taarifa katika baadhi ya vyombo vya habari kwamba, Tanzania imewarejesha nyumbani kwa nguvu, wakimbizi 25,000 wa Burundi mwezi mmoja uliopita. Vilevile serikali ya Tanzania imesema, taarifa hiyo ni ya uzushi ambayo haina ukweli wowote na yenye nia ya kuichafulia jina nchi ya Tanzania ambayo kwa muda mrefu imekuwa kimbilio na makaazi ya wakimbizi wengi kutoka nchi mbalimbali hasa za Ukanda wa Maziwa Makuu. Akizungumza na BBC, Mwakilishi Mkazi wa UNHCR nchini Tanzania , Bi. Joyce Mends Cole, amesema, amewasiliana na mwakilishi wa shirika hilo nchini Burundi ambaye amethibitisha kwamba hakuna wakimbizi wa nchi hiyo waliorejeshwa kutoka Tanzania. Bi. Joyce amebainisha kuwa, tatizo lililopo ni kuchanganywa kwa maneno "Wakimbizi" na "Wahamiaji Haramu". Amefafanua kwamba, katika operesheni inayoendelea kwa sasa nchini Tanzania, ya kuwasaka wahamiaji haramu huenda baadhi ya wakimbizi waliosalia wamekamatwa kimakosa. Hata hivyo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania Dk. Emmanuel Nchimbi, alimuhakikishia kuwa operesheni hiyo inafanyika kwa umakini mkubwa na kwa kuzingatia mikataba ya kimataifa ya haki za uhamiaji. #BBC
Posted on: Sat, 14 Sep 2013 03:58:30 +0000